1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

Putin anaelekea Beijing kuimarisha ushirikiano na China

19 Mei 2026

Rais wa Urusi Vladimir Putin anasafiri kwenda China kukutana na kiongozi wa China Xi Jinping ikiwa ni chini ya wiki moja baada ya Rais wa Marekani Donald Trump kukamilisha ziara yake mjini Beijing.

https://p.dw.com/p/5DwyN
Rais Putin na Xi wakikagua gwaride la kuadhimisha miaka 80 ya kumalizika kwa Vita Kuu ya Pili ya Dunia
Putin alizuru China mara ya mwisho mnamo Septemba 2025 Picha: Sergei Bobylev/TASS/ZUMA/picture alliance

Putin amepangwa kuwa nchini China Jumanne na Jumatano katika ziara ambayo huenda ikafuatiliwa kwa karibu wakati Beijing ikijitahidi kudumisha uhusiano thabiti na Marekani na wakati huo huo pia ikidumisha uhusiano imara na Urusi. Ikulu ya Kremlin imesema Putin na Xi wanapanga kujadili ushirikiano wa kiuchumi kati ya nchi hizo mbili, lakini pia "masuala muhimu ya kimataifa na kikanda." Ziara hiyo inaambatana na maadhimisho ya miaka 25 ya Mkataba wa Urafiki kati ya China na Urusi uliosainiwa mwaka wa 2001. Putin alizuru China mara ya mwisho mnamo Septemba 2025 kuhudhuria mkutano wa kilele wa kila mwaka wa Jumuiya ya Ushirikiano ya Shanghai huko Tianjin, kutazama gwaride la kijeshi linaloadhimisha kumbukumbu ya miaka 80 ya kumalizika kwa Vita vya Pili vya Dunia na kufanya mazungumzo na Xi.

Msemaji wa Kremlin Dmitry Peskov alisema mwishoni mwa wiki kwamba ziara ya Putin pia itairuhusu Urusi kupokea taarifa mpya za moja kwa moja na kubadilishana mawazo na China kuhusu mazungumzo yake na Marekani. Wakati wa ziara ya Trump, Xi alielezea uhusiano wa pande mbili kati ya Marekani na China kama muhimu zaidi duniani na akasema wanapaswa kuchukuliana kama washirika badala ya wapinzani. Kufikia mwisho wa mkutano huo wa siku mbili, nchi hizo zilisema zitaufanyia kazi mfumo mpya wa kusimamia "uhusiano mzuri wa utulivu na kimkakati kati ya China na Marekani."