Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza la Usalama la UN lakutana kwa dharura kujadili DRC

Bintou Keita (kwenye skrini), Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini humo, akihutubia wajumbe wa Baraza waliokutana kwenye kikao cha dharura kufuatia kuzidi kuzorota kwa hali ya usalama nchini DRC.
UN
Bintou Keita (kwenye skrini), Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini humo, akihutubia wajumbe wa Baraza waliokutana kwenye kikao cha dharura kufuatia kuzidi kuzorota kwa hali ya usalama nchini DRC.

Baraza la Usalama la UN lakutana kwa dharura kujadili DRC

Amani na Usalama
  • M23 wametwaa mji wa Kamanyola jimboni Kivu Kusini
  • Tayari wametwaa Goma, Kivu Kaskazini na Bukavu Kivu Kusini
  • M23 wameteua viongozi wao akiwemo Gavana na Meya

Wajumbe wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, mchana wa Jumatano ya Februari 19 wamejulishwa kile ambacho waasi wa M23 wanaoungwa mkono na Rwanda wanafanya baada ya kutwaa miji mikuu ya jimbo la Kivu Kaskazini na Kivu Kusini, Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC.

Akihutubia wajumbe wa Baraza waliokutana kwenye kikao cha dharura kufuatia kuzidi kuzorota kwa hali ya usalama nchini DRC, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini humo, Bintou Keita amesema M23 wameanzisha mamlaka yao.

Walinda amani wa Umoja wa Mataifa wakipiga doria Goma mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo baada ya mji huo kuzidiwa na waasi. Hapo mbele, sare za kijeshi na vifaa vimeachwa barabarani.
MONUSCO/Aubin Mukoni
Walinda amani wa Umoja wa Mataifa wakipiga doria Goma mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo baada ya mji huo kuzidiwa na waasi. Hapo mbele, sare za kijeshi na vifaa vimeachwa barabarani.

“Licha ya miito mingi ya kimataifa ya kusitisha mapigano na kukomesha mashambulizi, M23, imeendelea kusonga mbele katika majimbo  ya Kivu Kaskazini na Kivu Kusini. Hatua hizi zimekuwa na athari mbaya, zikisababisha kupoteza maisha ya watu wengi wakati M23 walipokuwa wanatwaa udhibiti wa Goma,” amesema Bi. Keita akihutubia wajumbe kwa njia ya video kutoka Kinshasa, mji mkuu wa DRC.

Ameendelea kusema kuwa “katika kipindi cha wiki mbili, Muungano wa Mto Congo, AFC ambao M23 ni moja ya sehemu zake kuu, umeanzisha utawala wake huko Goma kwa kuteua Gavana wa jimbo la Kivu Kaskazini pamoja na Meya wa mji wa Goma,”

Halikadhalika tarehe 16 Februari, M23 waliteka Uwanja wa ndege wa Kavumu pamoja na mji wa Bukavu ambao ni mji mkuu wa jimbo la Kivu Kusini.

“Na wameendelea kusonga mbele na jana waliteka mji wa Kamanyola, ambao uko katika eneo linalounganisha mipaka ya nchi tatu ambazo ni DRC, Rwanda, na Burundi,” amesema Bi. Keita ambaye pia ni Mkuu wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini, DRC, MONUSCO.

Haki za kibinadamu za wasichana na wanawake zinasiginwa

Bi. Keita amesema mashambulio ya M23 huko jimboni Kivu Kaskazini na Kivu Kusini yameongeza hatari kwa wasichana na wanawake kukumbwa na ukatili wa kijinsia na unyanyasaji wa kingono unaotokea kwenye maeneo yenye mizozo.

Wanawake wajawazito na wanaonyonyesha pamoja na watoto wanafaidika na chakula chenye lishe bora cha WFP ili kukabiliana na utapiamlo.  Wako kwenye foleni wakisubiri mgao wa wao chakula wa kila mwezi kwa mwezi wa Agosti 2024.
UN News/George Musubao
Wanawake wajawazito na wanaonyonyesha pamoja na watoto wanafaidika na chakula chenye lishe bora cha WFP ili kukabiliana na utapiamlo. Wako kwenye foleni wakisubiri mgao wa wao chakula wa kila mwezi kwa mwezi wa Agosti 2024.

“Watu kulazimika kukimbia, kuongezeka kwa wapiganaji wafungwa na kusambaa kwa silaha kunaongeza hatari hiyo,” amesema.

Kama hiyo haitosho, vikwazo vya kufikisha vifaa vya usaidizi vimeendelea kukwamisha uwezo wa Umoja wa Mataifa kutoa huduma kwa wahitaji.

Amesema wWahudumu wa kibinadamu lazima waendelee kuwa na uwezo wa kufanya kazi zao bila vizuizi ili wasaidie raia walioko hatarini.

Bi. Keita apatia  Baraza jukumu

"Ni muhimu kwamba Baraza hili lichukue hatua za haraka na za uamuzi ili kuzuia vita hivi visigeuke na kuwa vya kikanda,” amesema Bi. Keita akiongeza kuwa, “ninatoa wito kwa Baraza hili kuwawajibisha wahusika wa ukiukaji wa haki za binadamu na unyanyasaji katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.”

Pongezi kwa hatua ya Baraza la UN la Haki za Binadamu

Amesema katika muktadha huo “ninakaribisha hatua ya tarehe 7 mwezi huu wa Februari ya Baraza la Umoja wa Mataifa la haki za binadamu ya kupitisha azimio linaloanzisha Tume ya Kusaka Ukweli ambayo itafuatwa na Tume Huru ya uchunguzi  kuhusu ukiukaji wa haki za binadamu na sheria za kimataifa za kibinadamu huko mashariki mwa DRC.”

Wakimbizi wa ndani wakiwa kwenye eneo la kuteka maji lililoandaliwa na UNICEF kwenye viunga vya mji wa Goma,jimboni Kivu Kaskazini, nchini DRC.
© UNICEF/Jospin Benekire
Wakimbizi wa ndani wakiwa kwenye eneo la kuteka maji lililoandaliwa na UNICEF kwenye viunga vya mji wa Goma,jimboni Kivu Kaskazini, nchini DRC.

Wito kwa pande kinzani DRC

Hatimaye, ametoa wito kwa pande zote kutimiza majukumu yao ya kulinda raia kwa mujibu wa sheria za kimataifa za kibinadamu na sheria za kimataifa za haki za binadamu. “Hii ni pamoja na kutoharibu maeneo na vifaa vya Umoja wa Mataifa nchini DRC, ikiwa ni pamoja na usalama wa watu wanaolindwa na MONUSCO.

Matokeo ya kikao cha pamoja cha EAC na SADC

Bi. Keita ametumia hotuba yake pia kuonesha mshikamano na kilichoamuliwa kwenye kikao cha pamoja cha viongozi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, EAC na Jumuiya ya Maendeleo ya nchi za Kusini mwa Afrika, SADC kuhusu hali mashariki mwa DRC kilichofanyika tarehe 8 Februari nchini Tanzania.

Tweet URL

“Mkutano huo umesisitiza umuhimu wa kurejelea mazungumzo ya moja kwa moja na majadiliano na pande zote za kiserikali na zisizo za kiserikali, ikiwa ni pamoja na M23, ndani ya michakato ya Luanda na Nairobi,” amesema Bi. Keita, akinukuu ya kwambam mkutano pia  umerejelea hitaji la kutokomeza kikundi cha waasi cha FDLR na kuondolewa kwa majeshi ya Rwanda kutoka ardhi ya DRC.

“Ni muhimu kwamba masharti ya tamko la mkutano wa EAC-SADC kuhusu urejeshaji wa huduma muhimu za umma, kufunguliwa kwa uwanja wa ndege wa Goma bila kuchelewa, pamoja na njia kuu za kusambaza umeme, zikiwemo zile za Ziwa Kivu, yatekelezwe mara moja ili kupunguza mateso ya wananchi,” amesema Mkuu huyo wa MONUSCO

Amesema kwa upande wake, Umoja wa Mataifa, ukiwemo MONUSCO, umejizatiti kuunga mkono juhudi zozote zinazolenga kurejesha pande husika kwenye meza ya mazungumzo ili kupata suluhisho la kisiasa la kudumu kwa mgogoro huo, ambao unahatarisha uthabiti wa kanda nzima.

Amesema kwa muktadha huo, “ni muhimu kukumbuka mafanikio makubwa yaliyopatikana katika miezi ya hivi karibuni chini ya mchakato wa Luanda. Ni jambo la msingi, kama ilivyoainishwa kwenye tamko la mkutano wa Baraza la Amani na Usalama la Muungano wa Afrika, AU, uliofanyika Addis Ababa tarehe 14 Februari, kuhakikisha kwamba mafanikio haya hayapotei.

Mjumbe Maalum wa Maziwa Mkuu asema ‘historia inajirudia’

Tweet URL
Mjumbe Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa Ukanda wa Maziwa Makuu Huang Xia ameelezea hali iliyoko nchini DRC, akitaja tukio la mwishoni mwa mwezi Januari, kwamba “ni historia inayojirudia na inayochukiza’” akirejelea wakati Vuguvugu la tarehe 23 Machi au M23 wakiungwa mkono na jeshi la ulinzi la Rwanda, kwa mara nyingine tena waliposhambulia Goma.
 
“Lazima tuchukue hatua sasa,” ameonya Bwana Huang akisema tena kwa haraka, kwa pamoja na kwa kujizatiti.

Hivyo ametaja maeneo matatu muhimu ya kuzingatia:

  • Kumaliza uhasama kupitia sitisho la haraka la mapigano na pande zote ziheshimu ahadi zao kwenye Mifumo ya Kikanda na Kimataifa ikiwemo ule wa Addis Ababa. Kumaliza ghasia ni suala la dharura ili kuweza kushughulikia mahitaji ya kibinadamu, na kurejesha mazingira rafiki kwa mazungumzo ya kina kuanza.
  • Kurejesha mazungumzo akisema jawabu si kupitia jeshi bali mazungumzo ya kisiasa. Mazungumzo na kulegeza msimamo ni ni muhimu ili kufikia suluhisho la kudumu.
  • Mfumo wa pamoja wa kikanda wa kutatua mzizi wa mzozo mashariki mwa DRC, kwa kujumuisha mipango ya kati na ya muda mrefu huku wakiendelea kuchechemua Mfumo wa Addis Ababa ili kumaliza kabisa chanzo cha mzozo wa DRC.

 

Kauli ya DRC

Akizungumza kwa niaba ya mamlaka za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Waziri wa Mambo ya Nje, Thérèse Kayikwamba Wagner ameeleza mifano ya maelfu ya vifo vya kikatili na majeruhi huko Goma wakati wa mapigano na milipuko ya magonjwa inayotishia maisha ya wengi. Haya, amesema, ni matokeo ya kutekwa kwa Goma na aliloliita kundi la la kigaidi, na kwamba hayo yanafanyika machoni pa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa “ambalo halichukui hatua.”

Bi. Wagner amebainisha kuwa Jumuiya za kikanda za Afrika – Umoja wa Afrika, Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), na Jumuiya ya Kiuchumi ya Nchi za Afrika ya Kati (ECCAS) – yamekemea uwepo wa wanajeshi wa Rwanda katika DRC.
 
Waziri wa Mambo ya Nje, Thérèse Kayikwamba Wagner wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo akihutubia mkutano wa Baraza la Usalama kuhusu hali kataika nchi yake.
UN Photo/Evan Schneider
Waziri wa Mambo ya Nje, Thérèse Kayikwamba Wagner wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo akihutubia mkutano wa Baraza la Usalama kuhusu hali kataika nchi yake.
Aidha, amekaribisha uamuzi wa Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa wa kuanzisha tume ya uchunguzi kuhusu ukiukwaji wa haki za binadamu mashariki mwa DRC, pamoja na azimio la Bunge la Ulaya la kusitisha makubaliano kati ya Muungano wa Ulaya na Rwanda kuhusu uchimbaji wa madini muhimu.
 
Hata hivyo, amesema kuwa ni Baraza la Usalama pekee linaloweza kuzuia mauaji mapya na upanuzi wa eneo lililokaliwa kimabavu, akihimiza hatua madhubuti za kusitisha ghasia zinazofanywa na kundi la M23 na wanajeshi wa Rwanda, na “kukomesha msaada wa Nchi Mwanachama wa Umoja wa Mataifa kwa kundi la kigaidi linalojaribu kupindua serikali halali iliyochaguliwa kidemokrasia.”

Wekeni vikwazo kwa makamanda na wanasiasa wa Rwanda

“Baraza linapaswa kuweka vikwazo maalum kwa makamanda wa Jeshi la Ulinzi la Rwanda na viongozi wa kisiasa, pamoja na kupiga marufuku kabisa uuzaji wa madini yanayopewa lebo ya uwongo kuwa yametoka Rwanda,” amesema, akibainisha kuwa biashara hiyo imechochea vita katika mashariki mwa DRC kwa miongo kadhaa.
 
Kiongozi huyo mwanasiasa mashuhuri ametoa wito kwa Baraza la Usalama kufuta mara moja hadhi ya Rwanda kama nchi inayochangia vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Mataifa na kufuatilia kwa karibu uuzaji wa silaha kwa taifa hilo.
 
Ingawa kumekuwa na mikutano mitatu ya Baraza ndani ya mwezi mmoja, huku Rwanda ikilaaniwa kwa kauli moja, bado hakuna azimio lililopitishwa, amesema. Kwa hivyo, DRC inataka azimio linalokemea uvamizi wa Rwanda na kutaka kuondolewa kwa wanajeshi wake kutoka nchini humo.

Kauli ya Rwanda

Kwa upande wake Balozi wa Rwanda, Ernest Rwamucyo, ambaye ni Mwakilishi wa Kudumu wa Rwanda katika Umoja wa Mataifa, ameliambia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuwa hatua za  kijeshi za DRC na uandikishaji wa makundi yasiyo ya kawaida ya wapiganaji vimeunda “mazingira yasiyo na sheria,” na kuzidisha hali ya machafuko katika eneo hilo.
Nyumba moja huko Ihusi huko Kivu Kusini mashariki mwa DR Congo ilishambuliwa kwa bomu wakati wa mapigano kati ya waasi wa M23 na vikosi vya serikali.
© Les religieux de Ihusi
Nyumba moja huko Ihusi huko Kivu Kusini mashariki mwa DR Congo ilishambuliwa kwa bomu wakati wa mapigano kati ya waasi wa M23 na vikosi vya serikali.

Afrika kwa ajili ya Afrika

Amelaani hatua ya Kinshasa kujitoa kwenye mchakato wa amani wa kikanda, akisisitiza kuwa suluhu zinazoongozwa na Waafrika ndizo zinazopaswa kuwa mstari wa mbele katika juhudi za kumaliza mgogoro huo.
 
“Wakati nchi inapozidisha usambazaji wa silaha kwa makundi yenye silaha hasi, kinachopatikana ni machafuko,” amesema Balozi Rwamucyo, akionya kuwa silaha zinagawiwa kwa watoto huku mahitaji ya kibinadamu yakiongezeka.
 
Aidha, amelaani uvamizi wa eneo la Rwanda mnamo tarehe 29 Januari mwaka huu wa 2025, ambapo zaidi ya mamluki 200 wa kigeni waliripotiwa kuingia pamoja na jeshi la Congo, akielezea tukio hilo kama tishio kubwa kwa usalama wa taifa, ambalo limepuuzwa na jumuiya ya kimataifa.
 
Huku akikaribisha matokeo ya mkutano wa viongozi wa kikanda uliofanyika tarehe 8 Februari nchini Tanzania, ambao ulitoa wito wa kusitishwa kwa mapigano na misaada ya kibinadamu, amehimiza DRC kurejea katika mifumo ya kikanda ya usuluhishi. Pia ametoa wito kwa jumuiya ya kimataifa kupinga uingiliaji wa kijeshi kutoka nje na taarifa potofu ambazo, kwa mujibu wake, zinachochea mgogoro huo.